Al-kashaafu (Mwangaza) Katika Adabu Za Itikafu

Kitabu hiki kina zungumzia Mwangaza kuhusu ibada ya kukaa itikafu, maana yake adabu zake na masharti ya itikafu na faida zake, pia kimelezea sehemu na wakati wa itikafu, na itikafu ya mfanya kazi na makosa ya wanaofanya itikafu.

Al-kashaafu (Mwangaza) Katika Adabu Za Itikafu

[ Kiswahili - Swahili -السواحيلية ]

 


    
        
Mtunzi:
Muhammad Swaleh Al-Munajid

Mfasiri:
Abubakari Shabani Rukonkwa
Kimerejewa na:
Yunus Kanuni Ngenda

 

الكشاف في آداب الاعتكاف
    
    
المؤلف:
محمد صالح المنجد





المترجم:
أبوبكر شعبان روكونكوا
المراجع:
يونس كنون نغندا
Al-kashaafu (Mwangaza) Katika Adabu Za Itikafu


Kila sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu aliye juu mwingi wa kusamehe, sala na salamu ziwe juu ya Mtume wake mteule, na ziwe juu ya watu wake na maswahaba zake, na wote waliokuja baada yao, amma baad.
Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu ameweka baadhi ya masiku kuwa bora kuliko mengine, na hakuna msimu wowote ulio bora ila Mwenyezi Mungu anaweka wadhifa bora wa kumtii, basi mtu mwenye mafanikio ni yule anaeitumia nafasi ya misimu ya miezi, masiku na masaa, na akajikurubisha kwa Mola wake ndani ya masiku hayo, kwa kufanya twaa, huenda akapata mafanikio ndani ya masiku hayo, ambayo yatampa amani kutokana na moto wa jahanam.
Na miongoni mwa matendo makubwa yaliyo bora katika masiku kumi ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhan:
Itikafu: Mwenyezi Mungu ameitaja katika aya za swaum, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Wala msichanganyike nao (msiwaingilie), na hali mnakaa Itikafu msikitini. Hiyo ni mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi msiikaribie. Namna hivi Mwenyezi Mungu anabainisha Ishara zake kwa watu ili wapate kumcha}. (Al-baqrah: 187).
Kisha akausia kwamba Misikiti isafishwe kwa ajili ya itikafu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na tuliagana na Ibrahim na Ismail: Itakaseni Nyumba yangu kwa ajili ya wanao izunguka kwa kut'ufu na wanao jitenga huko kwa ibada, na wanao inama na kusujudu}. (Al-baqrah: 125).
Na alikuwa Mtume (s.a.w) yanapoingia masiku kumi ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhan anafunya juhudi katika ibada na anajitenga na wake zake na anawaamsha watu wake kwa ajili ya swala, na alikuwa hamuachi yeyote katika watu wake mwenye uwezo wa kusimama usiku ila alikua anamuamsha, na akikesha kwa kuswali na kumtaja Mwenyezi Mungu na kusoma Qur'an, na alikuwa anaongeza juhudi katika kufanya ibada zaidi ya ilivyokuwa kawaida yake, na alikua akijitahidi katika masiku hayo kwa ibada zaidi ya alivyokuwa akijitahidi katika masiku mengine, na alikuwa akikaa itikafu msikitini kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mola wake.
Maana ya Itikafu: Ni kulazimika kuwa msikitini na kukaa ndani yake kwa nia ya ibada na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Makusudio ya Itikafu: "Ni kuutuliza moyo kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na kuacha kujishughulisha na watu ili kujishughulisha na Mwenyezi Mungu peke yake, inakuwa akili yake yote na moyo wake wote viko kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na mawazo yake yote ni katika kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, na anafikiria ni jinsi gani atajikurubisha kwake na kupata radhi zake". Zadul-Maad.
"Kila yanapokuwa na nguvu maarifa ya kumjua Mwenyezi Mungu na kumpenda na kufurahika nae, basi mambo hayo yanamfanya mtu ajishughulishe na Mwenyezi Mungu moja kwa moja katika hali zake zote". Ibn Rajab, Latwaaif Al-maarif.
Na alikuwa Mtume (s.a.w) akikaa itikafu katika masiku kumi ya mwisho ya mwezi wa Ramadhan mpaka Mwenyezi Mungu alipomfisha, kisha wakakaa wake zake baada yake. Bukhar na Muslim.
Itikafu ni katika Sunna ambazo ni watu wachache sana wanaozifanyia kazi, amesema Ibn Shihaab Al-Zuhri Mwenyezi Mungu amrehem: (Maajabu yaliyoje ya waislamu! Wameacha itikafu pamoja na kwamba Mtume (s.a.w) hakuiacha tangu anafika Madina mpaka Mwenyezi Mungu anamchukua).
Na katika ibada hii kuna ubora na maana nyingi, na miongoni mwazo:
-Ni kufurahi kwa kuwa na Mwenyezi Mungu na kuwa nae faragha na kuelekea kwake.
-Ni kupata malezi ya kuipa nyongo dunia na kuifanya kuwa ndogo, na kuvumilia kutokana na kule kuiacha ladha ya usingizi na raha ya kitanda, na kujiweka mbali na starehe, na kumwelekea Mwenyezi Mungu na kujikurubisha kwake kwa kufanya aina tofauti za ibada.
-Miongoni mwa fadhila za itikafu, ni utulivu wa nafsi, na kusoma Qur'an na kuikhitimisha (kuimaliza), na kufanya toba ya kweli, na kusimama usiku, na kujizoesha kusimama usiku, na kuutumia vizuri wakati, na moyo kutengamaa na kuuweka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kuuhuisha kwa kutafakari na kuzingatia.
-Na miongoni mwa fadhila za itikafu, ni kuutafuta usiku wa Lailatul-qadir na kufaidika nao, na haya ni katika mambo matukufu anayoyatafuta mtu.
-Katika itikafu kuna kuulinda moyo kutokana na maneno mabaya, na kula na kunywa na kufanya tendo la ndoa na kujichanganya.
Sharti za Itikafu
Masharti ya itikafu ni kama yafuatayo:
*Mwenye kukaa itikafu awe ni mwenye kupambanua, haiswihi itikafu kwa mtoto mdogo ambae hawezi kupambanua.
*Awe ni mwenye kujitwaharisha kutokana na hadathi kubwa, (kutokana na janaba, hedhi na nifasi).
*Ajitenge na mambo yake yote ya kidunia, kama vile kutafuta pesa, kufanya biashara, kufanya kazi, kufanya tendo la ndoa na mengineyo.
*Itikafu iwe ni katika msikiti unaoswaliwa swala ya jamaa, ili asiiache swala ya jamaa kwa sababu ya itikafu, kwa sababu kujitenga kunakokata swala ya jamaa kumekatazwa.
Sehemu na wakati wa Itikafu
Misikiti inatofautiana katika ubora, unatangulizwa wenye malipo makubwa na wenye cheo cha juu, nao ni Msikiti mtukufu wa Makkah, na swala ndani ya Msikiti huo ni sawa na swala laki moja katika misikiti mingine, kisha Msikiti wa Mtume (s.a.w), na swala ndani yake ni sawa na swala elfu moja, kisha Masjid Al-Aqswa, na itikafu iliyokamilika ni ile inayofanywa ndani ya Misikiti hiyo mitatu, na ama Misikiti mingine ambayo inaswaliwa swala ya jamaa ndani yake, yote inafaa kukaliwa itikafu kwa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu inayosema: {Wala msichanganyike nao (msiwaingilie), na hali mnakaa Itikafu msikitini. Hiyo ni mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi msiikaribie. Namna hivi Mwenyezi Mungu anabainisha Ishara zake kwa watu ili wapate kumcha}. (Al-baqrah: 187).
Na kipimo cha misikiti kuwa bora kinarejea katika mambo yafuatayo:
-Msikiti kuwa wa zamani, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Msikiti ulio jengwa juu ya msingi wa uchamngu tangu siku ya mwanzo unastahiki zaidi wewe usimame ndani yake. Humo wamo watu wanao penda kujitakasa. Na Mwenyezi Mungu anawapenda wanao jitakasa}. Al-Tawba: 108).
-Msikiti ambao una idadi kubwa ya jamaa, amesema Mtume (s.a.w): (Na hakika swala ya mtu pamoja mtu mwingine ina utukufu zaidi kuliko ya mtu akiwa peke yake, na swala ya mtu akiwa na watu wawili ina utukufu zaidi kuliko akiwa na mtu mmoja, na ile yenye watu wengi ndiyo yenye kupendwa na Mwenyezi Mungu). Hadithi hii kaifanya kuwa nzuri Imamu Al-Baniy.
Kwakuwa lengo la itikafu ni kujitenga kwa ajili ya ibada na kuuweka moyo kwa Mwenyezi Mungu, basi anatakiwa mwenye kufanya itikafu achague msikiti wenye kumfaa ambao moyo wake utatengamaa akiwa ndani ya msikiti huo, hata kama sio Misikiti miwili mitukufu, (Msikiti wa Makkah na wa Madina), kuanzia hapo ndipo ikawa misikiti bora kwa mwenye kukaa itikafu ni ile ambayo moyo wake unapata unyenyekevu zaidi, na vinapatikana vitu ambavyo vinamfanya awe mnyenyekevu, kama vile: Kutokuwa na vishawishi sehem ya itikafu, kupatikana Imamu ambae atamuathiri katika kisomo chake na mawaidha yake.
Na vyumba vilivyoko ndani ya msikiti ambavyo milango yake iko wazi vinachukua hukumu ya msikiti, kwahiyo inajuzu kukaa itikafu ndani yake, kwa sababu ni sehem ya msikiti, ama (vyumba hivyo) vikiwa vimejengwa nje ya mipaka ya msikiti haijuzu kukaa ndani yake itikafu, na ijuzu kwa mwenye kukaa itikafu kuwahi nafasi yake katika msikiti kama vile chumba au sehem ya kona au mfano wake, kwa sharti kusiwe kuna madhara katika maslahi ya swala.
Na inajuzu kukaa (itikafu) katika sehem ambayo inahukumu ya msikiti kama vile ukumbi wa msikiti au uwanja wake na mfano wa hayo.
Na inajuzu kukaa itikafu sehemu yoyote, mwezi wa Ramadhan na miezi mingine, itikafu haina muda maalum bali imependekezwa katika muda wowote, na inatiliwa mkazo hasa wakati wa funga (swaum), na mwenye kuweka nadhiri ya kukaa itikafu ni wajibu kwake yeye kuitekeleza.
Na itikafu: "ni kukaa msikitini kwa ajili ya kumtii Mwenyezi Mungu, kwa muda mchache au muda mwingi, kwa sababu haikupokelewa dalili iliyohusisha muda maalum au siku nyingi au chache". (Majumuu Al-fataawa Ibn Baaz/15441).
Na itikafu iliyo bora ni kukaa itikafu masiku kumi yote ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhan, kwa sababu ndivyo alivyofanya Mtume (s.a.w).
Ikiwa hakuweza kukaa itikafu masiku yote kumi basi atakaa masiku atakayoweza hata kama ni siku moja.
Na atakaetaka kukaa itikafu katika masiku yote kumi ya mwezi wa Ramadhan ataingia sehem ya kukaa itikafu siku ya tarehe 20 kabla jua halijazama karibu na usiku wa tarehe 21, na hii ndio kauli ya jopo la wanachuoni, kwa hadithi ya Mtume (s.a.w): (Atakae kaa itikafu na mimi, basi aanze itikafu katika kumi la mwisho).
Na atamaliza itikafu baada ya kuzama jua siku ya mwisho ya mwezi Mtukufu wa Ramadhan, sawa ni tarehe 29 au tarehe 30.
Na ikiwa ni usiku wa shaka basi atasuburi mpaka ithibiti kwamba kesho ni siku ya kufungua, na akipata habari kwamba kesho ni siku ya kufungua atatoka akijua kwamba usiku ule ni usiku wa kuamkia iddi.
-Kuiandaa misikiti kwa ajili ya itikafu na kuisafisha pamoja na kuiwekea manukato, na kuwahudumia wenye kukaa itikafu ndani yake, ni katika ibada kubwa.
-Kujishughulisha na swala, kusoma Qur'an, kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, kufanya toba, kuihesabu nafsi, kuzingatia na kutafakari na mfano wa hayo.
-Atajiepusha na yale yasiyomuhusu miongoni mwa maneno na vitendo, na ajiweke mbali kutokana na maneno mengi.
-Ajiepushe na mijadala na maneno yasiyo na faida, na matusi, na matendo machafu, kwa sababu mambo hayo yamekatazwa katika wakati usiokuwa wa itikafu, basi katika ndio zaidi kabisa.
-Hakuna tatizo kuzungumza kwa haja na kuwazungumzisha wengine, na kufanya yale anayoyahitaji miongoni mwa mambo ya halali.
-Hakuna tatizo kukaa itikafu mtu na rafiki yake au ndugu yake wa karibu, pamoja na kuacha maneno yasiyokuwa na maana (qiila wa qaala), na kuacha malengo yasiyokuwa ya itikafu.
-Aliyekaa itikafu inatakiwa achunge adabu za kukaa msikitini na hukumu zake, ikwemo kupunguza sauti, na kacha makelele, kuuza na kutangaza vitu vilivyopotea, na achunge sunna ya tahiyatul masjid pindi anapotoka kwa ajili ya shida na akakaa nje sana kisha akarejea, tofauti na anapotoka kwa muda mchache haimlazim kuswali tahiyatul masjid, na inaruhusiwa kuchaji simu kwa haja.
-Kilicho bora kwa mwenye kukaa itikafu ni kuleta mahitaji yake kwa ajili ya itikafu yake, na asihudumiwe na mtu mwingine bali yeye awahudumie wengine.
-Mwenye kukaa itikafu akibana matumizi katika chakula (akila kidogo) inamfanya awe na uchangamfu na itampa muda wa kukaa peke yake.
Baadhi ya watu wanaacha kazi zao na nyadhifa zao na mambo ya wajibu wanayotakiwa kutekeleza ili wakae itikafu, na hii siyo sahihi kwa sababu anaenda kinyume na mkataba wa kazi, na hiyo ni haram, iweje aache jambo la wajibu kwa sababu Sunna, na mwenye kufanya hivo akaacha kazi yake aliyopewa na akakaa itikafu, basi anatakiwa aikate hiyo itikafu arudi kazini ili chumo lake liwe la halali.
Na inaharibika itikafu kwa kutoka msikitini bila ya haja yoyote.
Ama haja ambayo hana budi kuitekeleza, kama vile kwenda msalani, kuoga janaba na kula kama hakupata mtu wa kumletea chakula na mfano wake, basi inajuzu kwake yeye kutoka kwa ajili hiyo, na ajitahidi mahitaji anayoyataka yawe sehem ya karibu.
Na kanuni ya sheria hii inasema: Hakika mwenye kukaa itikafu haijuzu kwake yeye kuondoka msikitini isipokuwa kwa dharura na shida ambayo hana budi kuitimiza, basi ataitimiza kwa muda mchache kisha arudi.
Angalizo: "Haijuzu kuuza au kununua msikitini, kwa sababu hiyo ikiwa atahitaji kuagiza chakula kutoka hotelini itabidi atoke nje ya msikiti apige simu, kisha hakuna tatizo akipokea chakula akiwa msikitini na akalipa pesa, kwa sababu kufanya hivo ni kulipa deni, na imethibiti katika Sunna kuwa inajuzu kulipa deni ukiwa msikitini". Fataawah ya Shekh Abdul Rahman Al-Barrak.
Mwenye kukaa itikafu haruhusiwi kumtembelea mgonjwa wala kusindikiza jeneza wakati wa itikafu yake, wala haitikii wito (akialikwa), na wala hatekelezi shida za familia yake isipokua zile za dharura, na haruhusiwi kutoka kwenda kazini akiianza itikafu, na inajuzu kabla ya kukaa itikafu aweke sharti la kutoka kwa sababu isiyopingana na lengo la itikafu, kama vile kusema: nikipatwa na dharura au nikiugua, basi nitatoka msikini.
Na faida ya kuweka sharti ni kwamba, akitoka kwa sababu ya sharti aliloweka basi anaendelea kuwa katika hukumu ya waliokaa itikafu na malipo yake yanaendelea.
Akiugua wakati wa Itikafu: Ikiwa ni maradhi ya kawaida ambayo hayampi tabu kukaa msikitini, kama vile kichwa, maumivu ya jino na jicho na mfano hayo miongoni mwa magonjwa ambayo hayamlazim mtu kulala, basi haijuzu kwake yeye kutoka msikitini, kwa sababu anaweza akasubiri au akatumia baadhi ya dawa na yeye akiwa msikitini, basi kutoka kwake kunabatilisha itikafu yake.
Ama yakiwa ni maradhi makali kiasi kwamba anapata mashaka ya kukaa msikini kwakuwa anahitaji kulala na mtu wa kumhudumia, na matibabu, na vipimo vya daktari, na mfano wa hayo, katika hali hiyo ni halali kwake yeye kutoka kwakuwa anashida ya kutoka, na akipona atarejea msikitini na kuendelea na itikafu yake.
Na atakapopata hedhi mwanamke aliyekaa itikafu, ni wajibu kwake yeye kutoka msikitini.
Itikafu haibatiliki kwa kujiotea, bali atatoka na aoge kisha arudi msikitini, kwa sababu haijuzu kwa mwenye janaba kukaa msikitini, na itikafu yake haikatiki kwa kutoka kwake.
Na inajuzu kuhama msikiti kwenda msikiti mwingine kwa lengo la kupata ujira mkubwa zaidi, kama vile kuhamia katika Misikiti miwili mitukufu Makkah na Madina.
-Wala haibatiliki itikafu kwa kutolewa kwa lazima msikitini, kama ilivyo hali ya ndugu zetu madhaifu ambao misikiti yao inaripuliwa.
Itikafu ya Mfanyakazi
-Inapendeza kwa mfanyakazi achukue likizo ili afaidike katika kuutengeneza moyo wake kwa kukaa itikafu.
-Haiswihi kwa mwenye kukaa itikafu kuweka sharti la kwenda kazini, kwa sababu linapingana na malengo ya itikafu.
-Haiswihi kwa mwenye kukaa itikafu kwenda na laptop ili kufanya kazi zake ndani ya msikiti, na makatazo yanakuwa makubwa zaidi ikiwa ndani yake kuna kuuza na kununua, kama vile kufanya biashara katika soko la hisa na mfano wa hilo.
-Haijuzu kukaa itikafu ikiwa utaratibu na maslahi ya kazi vinakataza hilo.
-Ni juu ya mfanyakazi akae itikafu usiku nzima tangu kuzama kwa jua mpaka kuchomoza alfajiri, (na hii ni kauli ya baadhi ya wanachuoni), na katika likizo ya mwisho wa wiki inakuwa ni fursa kwa mwenye kutaka kuzidisha kukaa itikafu.
Itikafu ya Mwanamke
Itikafu vilevile ni Sunna kwa mwanamke, na wakeze Mtume Allah awaridhie walikuwa wakikaa itikafu pamoja na Mtume (s.a.w) katika maisha yake, na wakakaa itikafu baada ya kufa Mtume (s.a.w), na mwanamke wa kiislamu mwenye juhudi katika ibada atakaa itikafu kwa masharti yafuatayo:
-Apate idhini kwa mume wake au walii wake.
-Msikiti uwe umeandaliwa katika upande wa stara na hifadhi kwa mwanamke.
-Uwepo usalama wa kutosha na hasa nyakati za usiku.
-Kukaa kwake itikafu kusiwe kunapoteza haki za mume na watoto.
-Atakapo amrishwa na mume wake kutoka msikitini ni wajibu kwake yeye kumtii.
-Awe amejitwaharisha kutokana na hedhi, na ikimtokea hedhi akiwa katika itikafu ni wajibu kwake yeye kutoka na malipo yake ni kwa Allah.
-Kuwa na ikhlas na kutokujivuna.

Miongoni mwa faida za itikafu
-Kuwa na ikhlas na kuizoesha nafsi juu ya ikhlas, kwa sababu mwenye kukaa itikafu anakuwa faragha na Mola wake.
-Ni kupata malezi ya kuacha kuwa na maneno mengi ya upuuzi, na kula na kulala kuliko pindukia, na kujichanganya, na kuizoesha nafsi juu ya kuhifadhi muda, tumbo, ulimi na viungo.
-Ni amalezi ya ibada na hasa kusimama usiku na kusoma Qur'an, na kufanya adhkari, na kumuomba wokovu Mwenyezi Mungu.
-Ni kujenga mausiano ya nguvu na Mwenyezi Mungu, na kukimbilia kwake, na kumuomba wokovo.
-Ni kuukusanya moyo na kuyakusanya mawazo pamoja, na kuitumia akili kwa ajili ya maslahi ya akhera, na hii inasaidia na inafaida katika kukabiliana na fitna na shida.
-Ni kuirejea nafsi na kuihesabu, na kuyajua mapungufu na kuyatibu, hasahasa katika mambo ya ibada na msimamo katika mambo ya dini.
-Ni malezi ya kipekee juu ya kutumia muda na kuto kuupoteza.
-Ni kuihuisha Sunna hii kubwa ambayo watu wengi wameikimbia (sunna ya kukaa itikafu).
-Ni malezi juu ya kuwa na subira na kupigana na nafsi, na kuto kufuata matamanio ya nafsi na shetani.
-Ni kuhifadhi twahara na kuswali katika swafu ya kwanza, na kuipa takbira ya kuhirimia kila siku, na kupata Baraka ya kuwa pamoja katika ibada, na kuwaiga watu wema.
-Katika ibada ya itikafu kuna kutofautisha baina ya kukaa faragha na Mwenyezi Mungu kisheria, na kukaa faragha isiyokuwa kisharia, kama vile kukaa faragha kwa Mapadri katika mahekalu yao, na watu waliochupa mipaka na wazushi katika mapango na majangwa.
Miongoni mwa makosa wanayafanya baadhi ya wenye kukaa itikafu
-Kulala sana wakati wa mchana na kukesha usiku bila ya kufanya ibada, kiasi kwamba hakuna ibada anayoifanya isipokuwa swala tu.
-Kutoka msikitini ovyo bila ya haja yoyote.
-Ni kutumia kuliko kupita kiasi vifaa vya kisasa kama vile ipad, smart phone na laptop, kiasi kwamba moyo wake na fikra zake vinatoka msikitini na kuelekea katika dunia na mabonde yake hata kama kiwiliwili chake kipo msikitini, na wnengine wanafanya kazi zao na kuendesha biashara zao hali ya kuwa wamo ndani ya itikafu, na hakuna shaka kwamba kufanya hivo kunapingana na maana ya itikafu.
-Ni wingi wa kukutana na kuongea kwa muda mrefu baina ya wenye kukaa itikafu na wageni, mazungumzo yasiyokuwa ya ibada, na kujishughulisha na maneno mengi yasiyokuwa na faida, na kufanya mambo ya haram kama vile, kusengenya na kusema uongo, na mwenye kukaa itikafu ndie anaeonewa wivu kwa wakati wake na wageni wanao mshughulisha kutokana na kukaa kwake faragha kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.
-Ni kuzidisha kuleta vyakula na kuchafua busati la msikiti, na kuwaudhi wenye kuswali kutokana na harufu.
-Ni kudhani baadhi ya wenye kukaa itikafu kwamba kujipamba na kujitia manukato vinapingana na lengo la itikafu wanabakia kuwa katika hali ambayo inawaudhi wenye kuswali, na alikuwa Mtume (s.a.w) anakitoa kichwa chake dirishani hali ya kuwa yupo msikitini amekaa itikafu ili mke wake Aisha (r.a) azichane nywele zake.
-Ni kujishughulisha na kusoma au kufatilia matukio ambayo hayaendani na malengo ya itikafu na kujikuta anapoteza muda wake wa kukaa itikafu wenye thamani.
-Ni kukaa itikafu kwa lengo la kujifakharisha au kwa lengo lolote ambalo linapingana na makusudio ya itikafu, kama alivyokataza Mtume (s.a.w) katika kauli yake akisema: (Wanadhani kufanya hivo ni ibada?), Akikusudia waache kwani imekatazwa, na miongoni mwa mambo hayo ni kukusudia kuandaa vyakula vya aina tofauti ambavyo vinaletwa msikitini kwa ajili ya waliokaa itikafu, na miongoni mwa huduma za tofauti wanazopewa, na jambo lililo kamilika zaidi kwa watu wenye nia thabiti na imani ni kujiweka mbali na muonekano wa itikafu ya kifakhari, na kuwaachia mambo hayo wale ambao wajizoesha nafsi zao na ibada hiyo.
-Miongoni mwa watu kuna wanaokaa itikafu hali ya kuwa familia zao zinawahitaji, au wazazi wao wanawahitaji, watu kama hao itakuwa wanatekeleza Sunna na wanaacha wajibu, haijuzu kufanya hivo, na inamtosha mtu kupata madhambi kuwapuuzia wanaomuhitajia.


Mwisho
Alisema A'twaa Alkhurrasaan: "Mfano wa mtu aliyekaa itikafu ni kama fano wa mja aliyeiweka nafsi yake katika mikono ya Mola wake, kisha akasema: Ewe Mola wangu siondoki sehemu yangu mpaka unisamehe! Ewe Mola wangu siondoki sehemu yangu mpaka unihurumie".
Ewe Mola mja wako amekujia
Ametenda makosa mengi na amekosea
Inamtosha aibu yake kwako Wewe kutokana na matendo machafu aliyofanya
Amebeba madhambi juu ya madhambi
Yenye kuangamiza aliyoyatenda
Na amekuja kujikurubisha kwenye msamha wako kutokana na adhabu zako
Ewe Mwenyezi Mungu msamehe na umpe afya, kwa hakika Wewe ni mbora wa wenye kusamehe.
Na sala na amani ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad (s.a.w) na watu wake na maswahaba zake wote.